
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limesisitiza ushirikiano wa wadau wote wakiwemo Serikali, Sekta binafsi, taasisi za umma, jamii na wananchi katika kusimamia na kuhifadhi mazingira kwa maendeleo endelevu.
Akizungumza na waandishi wa habari tarehe 17 Juni, 2026 katika ukumbi wa mikutano wa NEMC Jijini Dar es salaam, Kaimu Meneja Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma NEMC, Bi. Martha Kawishe, amesema mazingira ni suala mtambuka linalohitaji kila mdau kutimiza wajibu wake kwa kuzingatia Sheria na Miongozo ya Mazingira iliyowekwa.

Ameeleza kuwa NEMC inaendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria kupitia ukaguzi wa miradi, utoaji wa elimu kwa umma katika masuala mazima ya udhibiti wa kelele chafuzi za mazingira, uharibifu wa vyanzo vya maji, utupaji holela wa taka, kutiririsha maji taka msimu wa mvua, ukataji hovyo wa miti na kuhakikisha miradi yote inazingatia Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) kabla ya kuanza.

Aidha, amewataka wananchi kuwa makini na watu wanaojifanya maafisa wa NEMC kwa lengo la udanganyifu, akisisitiza kuwa malipo yote hufanyika kwa utaratibu wa kiserakili na ukaguzi hufanywa na maafisa kisheria wakiwa na vithibitsho vifuatavyo: vitambulisho vya ukaguzi, vitambulisho vya kazi pamoja na nyaraka zinazompa mamlaka kisheria ya kufanya ukaguzi, na hasa ikizingatiwa ukaguzi hufanywa kidigitali ambapo mteja hupokea ujumbe mara baada ya ukaguzi.

NEMC pia imehimiza wananchi kutumia huduma rasmi ya kituo cha huduma kwa mteja kwa kupiga namba ya bure 0800110115 na kutumia mfumo wa e-mrejesho kwa kufuata menyu ya *152*00# na kufuata maelekezo ili kutoa ushauri, taarifa au changamoto za kimazingira.
Post a Comment