Na Mbuke Shilagi-KageraKatika maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika Juni 16,2026 Mkuu wa Wilaya ya Bukoba mkoani Kagera, Mhe. Erasto Siima, ameitaka jamii kutambua umuhimu wa malezi bora kwa watoto ili waweze kukua katika mazingira salama na yenye kuwajenga kimwili, kiakili na kimaadili.
Mhe. Siima amesema kuwa watoto wanapaswa kupata haki zao za msingi ikiwemo elimu, huduma za afya na malezi yenye maadili mema, jambo ambalo litasaidia kujenga taifa imara lenye maendeleo endelevu.
Amebainisha kuwa jukumu la kulea na kumlea mtoto si la wazazi pekee, bali ni wajibu wa jamii nzima kuhakikisha watoto wanalelewa katika mazingira bora
Aidha, amesema kuwa katika Manispaa ya Bukoba kumekuwa na juhudi mbalimbali zinazotekelezwa kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha mtoto anakua katika maadili mema kuanzia akiwa tumboni mwa mama yake hadi kufikia umri wa chini ya miaka nane.
Akizungumzia suala la ulinzi wa mtoto, Mkuu huyo wa Wilaya amesema Manispaa ya Bukoba imeendelea kupambana na vitendo vya ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto kwa kutoa elimu katika shule zote za msingi na sekondari inayolenga kuwajengea watoto uelewa kuhusu haki zao na namna ya kujilinda dhidi ya vitendo vya ukatili.
Vilevile, amewaagiza viongozi na watendaji wa Manispaa ya Bukoba kuendelea kutoa elimu mashuleni kwa kushirikiana na Dawati la Jinsia na Watoto ili wanafunzi waendelee kuelewa haki zao, kuzitambua na kuzitetea wanapokumbana na changamoto mbalimbali.
Kauli hiyo imekuja wakati ambapo tmTaifa linaendelea kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika, siku inayolenga kuhamasisha ulinzi, ustawi na maendeleo ya watoto barani Afrika.









إرسال تعليق